Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, amewataka Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kusimamia kwa umakini ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kuwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa wilayani humo.
Mheshimiwa Itunda ametoa wito huo wakati akihutubia kikao cha pili cha ufunguzi wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya (Mbeya DC), kilichofanyika leo, tarehe 03 Februari 2026.
Amesema kuwa Madiwani wanapaswa kushirikiana kwa karibu na Watendaji wa Serikali katika ngazi ya kata na vijiji ili kuimarisha juhudi za ukusanyaji wa mapato ya ndani, kwa lengo la kufikia asilimia 100 ya makusanyo ifikapo mwezi Juni 2026.
Aidha, DC Itunda amesisitiza umuhimu wa Madiwani kusimamia kwa karibu matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo zinazotolewa na Serikali Kuu, hususani miradi mikubwa ya kimkakati, ili kuhakikisha thamani ya fedha inazingatiwa katika kila mradi unaotekelezwa kwenye kata zao.

Akizungumzia miradi hiyo ya kimkakati, DC Itunda amesema Serikali tayari imetoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya njia nne kutoka Kata ya Igawa hadi Tunduma yenye thamani ya shilingi bilioni 183. Awali, mradi huo ulikuwa na thamani ya shilingi bilioni 128, lakini Serikali iliongeza shilingi bilioni 55 ili kuimarisha utekelezaji wake.
Vilevile, Serikali imetoa shilingi bilioni 119 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa maji kutoka Kata ya Kiwira, iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, ambao unalenga kumaliza changamoto ya maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya na Halmashauri ya Jiji la Mbeya. Kwa sasa, mradi huo umefikia asilimia 50 ya utekelezaji wake.
DC Itunda ameongeza kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imefanikiwa kutekeleza zoezi la kupeleka umeme vijijini kwa asilimia 95, hatua itakayosaidia wananchi kupata nishati safi na bora kwa ajili ya maendeleo ya shughuli mbalimbali za kiuchumi.
Kwa upande mwingine, amebainisha kuwa Serikali imetoa shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya ujenzi wa jengo jipya la Halmashauri, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.