Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, amewataka Watendaji wa Serikali hususani Watendaji wa Kata (WEOs) na Vijiji (VEOs) kushirikiana kikamilifu katika kusimamia utekelezaji wa Mpango wa Chakula Shuleni ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya (Mbeya DC).
Mhe. Itunda ametoa agizo hilo leo wakati wa kufunga Kikao cha Kamati ya Ushauri ya Halmashauri ya Wilaya (DCC), kilichoketi kujadili na kupitisha Rasimu ya Mapendekezo ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027.
Katika Rasimu ya Bajeti hiyo, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imepanga kukusanya na kutumia jumla ya shilingi bilioni 72.4 kutoka vyanzo mbalimbali, ikiwemo mapato ya ndani na ruzuku ya Serikali kwa ajili ya kugharamia mishahara, matumizi ya kawaida (OC), miradi ya maendeleo, pamoja na vyanzo fungiwa kama 'CHF', 'User Fee', 'NHIF' na Michango ya Jamii.
Sambamba na hilo, Mhe. Itunda amesisitiza umuhimu wa kuwashirikisha wazazi kikamilifu ili wachangie Mpango wa Chakula Shuleni. Hatua hiyo inalenga kuboresha afya za wanafunzi na kuongeza ufanisi wao katika kujifunza, hususani wakati wa masomo ya mchana.
“Tayari tumefikia asilimia 89 ya utekelezaji wa Mpango wa Chakula Shuleni. Nasisitiza Watendaji wa Kata na Vijiji, kwa kushirikiana na Madiwani, muendelee kusimamia jambo hili kwa umakini. Pia naelekeza wazazi wachangie chakula shuleni. Kama mzazi anaweza kumudu chakula cha mtoto wake nyumbani, kwa nini ishindikane shuleni? Sehemu ya chakula anachokula mtoto nyumbani, mzazi aichangie shuleni. Hatuhitaji fedha; tunahitaji chakula,” ameeleza Mhe. Itunda.
Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.