MBEYA DC YAPOKEA VIFAA KUWEZESHA MASIJALA MTANDAONI
Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imekabidhi vifaa vya kielektroniki, ikiwemo kompyuta tano (5) za kisasa za mezani pamoja na printa tano (5), kwa ajili ya kuimarisha utekelezaji wa mfumo wa masijala mtandaoni (e-Registry).
Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kuendeleza utekelezaji wa shughuli za Serikali mtandaoni (e-Government) katika halmashauri hiyo.
Hafla ya makabidhiano ya vifaa hivyo imefanyika leo, tarehe 03 Februari 2026, wakati wa ufunguzi wa kikao cha pili cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, inayoundwa na kata zipatazo 28.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica Yegella, amesema kuwa ununuzi wa vifaa hivyo umegharimu jumla ya shilingi milioni 24.
Ameeleza kuwa vifaa hivyo vina umuhimu mkubwa katika kuboresha utekelezaji wa majukumu ya Serikali kwa njia ya mtandao, sambamba na kupunguza matumizi ya karatasi, hatua itakayochangia uhifadhi wa mazingira.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Aidda Clemence Haule, amemshukuru Mkurugenzi Mtendaji kwa kusimamia kwa ufanisi manunuzi ya vifaa hivyo, akibainisha kuwa vitasaidia kuongeza tija na ufanisi wa utendaji kazi wa shughuli za Serikali mtandaoni, ikilinganishwa na mfumo wa awali uliotegemea zaidi matumizi ya karatasi.

Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.