Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya (Mbeya DC), Bi. Erica Yegella, leo amefanya kikao kazi maalum na Watendaji wa Vijiji (VEOs) kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji, ikiwemo fursa zilizopo, changamoto zinazowakabili, pamoja na mikakati ya kukabiliana nazo ili kuharakisha maendeleo kwa wananchi.
Katika kikao hicho, Bi. Yegella aliwasisitiza Watendaji wa Vijiji kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma. Aliwataka kuwa na unyenyekevu na kuwaheshimu Wenyeviti wa Vijiji, ambao ni wawakilishi halali wa wananchi katika maeneo yao.
“Niwaombe tuwaheshimu sana Wenyeviti wa Vijiji. Tufanye kazi kwa unyenyekevu na upendo, kwa sababu unyenyekevu ni sifa muhimu ya kiongozi. Kumbukeni kuwa ninyi ni wasimamizi wakuu katika vijiji vyenu; vitongoji vyote vinawategemea na kuwasikiliza. Msipokuwa wanyenyekevu, wenye utii na kuheshimu viongozi wenzenu, itakuwa vigumu kutekeleza majukumu yenu ipasavyo,” alieleza Mkurugenzi Mtendaji huyo.

Bi. Yegella alisisitiza zaidi kuwa Watendaji wa Vijiji ni kiungo muhimu kati ya Halmashauri na wananchi katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo. Hivyo, aliwataka kujiepusha na mambo yasiyo ya msingi na badala yake kutimiza wajibu wao kwa weledi na uwajibikaji.
Alielekeza kwamba pale wanapokumbana na changamoto au kutoelewa jambo, wawasiliane kwanza na Watendaji wa Kata; na endapo nao watashindwa kutoa ufafanuzi, basi wawasiliane na Watumishi wa Idara ya Utawala na Utumishi ngazi ya Halmashauri.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi huyo aliwahimiza Watendaji wa Vijiji kutumia ipasavyo mifumo ya kidijitali katika malipo na usimamizi wa fedha, ili kurahisisha uandaaji wa hesabu, hususani mwishoni mwa mwaka wa fedha. Alisisitiza kuwa kila Mtendaji wa Kijiji anapaswa kuielewa vizuri mifumo ya malipo, kwa kuwa wao ndio wasimamizi wakuu wa shughuli za kiutawala na kifedha katika vijiji.
“Sasa hivi hatufanyi malipo kwa mkono kwa kutumia makaratasi. Kila kitu kinafanyika kupitia mifumo ya kidijitali. Hata mishahara hailipwi tena kwa kupanga foleni kama ilivyokuwa zamani wakati wa matumizi ya stakabadhi za kuandika kwa mkono (HW5),” alifafanua Mkurugenzi huyo.
Akihitimisha kikao hicho, aliwataka Watendaji wa Vijiji kuhakikisha hawatoi fedha benki bila kuwa na nakala ya muamala kutoka katika mfumo wa FFAIRS pamoja na muhtasari wa kikao husika. Alisisitiza kuwa hatua hiyo ni ya lazima, na kwamba mihtasari ya vikao vyote vya kamati lazima iambatane na nakala kutoka kwenye mfumo ili kuruhusu utoaji wa fedha.

Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.