Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya (Mbeya DC), Mheshimiwa Aidda Haule, leo amekabidhi vishikwambi 44 vyenye thamani ya shilingi milioni 26.4 kwa madiwani wa halmashauri hiyo, kama sehemu ya vitendea kazi vitakavyotumika katika shughuli za Baraza la Madiwani.

Ugawaji wa vishikwambi hivyo umefanyika wakati wa Baraza la Madiwani Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya liliketi kujadili na kupitisha Rasimu ya Mapendekezo ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027. Hatua hiyo imefuatia Kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) kilichofanyika Februari 10, 2026, ambacho kilijadili na kupitisha rasimu hiyo kabla ya kuwasilishwa katika Baraza la Madiwani.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Haule amesema kuwa, lengo la kugawa vishikwambi hivyo ni kupunguza matumizi ya karatasi na kuimarisha matumizi ya mifumo ya kielektroniki katika kuandaa, kuhifadhi na kutumia taarifa za vikao. Ameeleza kuwa matumizi ya teknolojia yataongeza ufanisi, wepesi na usalama wa taarifa muhimu za Halmashauri.

Aidha, amesisitiza kuwa nyaraka zitakazohifadhiwa katika vishikwambi hivyo ni taarifa muhimu na za siri, zinazolindwa kwa mujibu wa sheria na kanuni za utumishi wa umma. Ameonya kuwa ni kosa kubwa kwa mtu yeyote kusambaza taarifa hizo kabla hazijajadiliwa, kupitishwa na kuazimiwa rasmi na Baraza la Madiwani kuwa za wazi kwa umma.
“Nyaraka zitakazowekwa katika kishikwambi hicho ni siri. Hupaswi kumweleza hata mwenza wako. Wewe ni mtumishi wa umma, umekula kiapo cha utumishi wa umma; hivyo, ni wajibu wako kuishi kwa kuzingatia kiapo hicho katika kipindi chote cha utumishi wako,” amesisitiza Mheshimiwa Haule.

Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.