Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya (Mbeya DC) leo imepitisha Rasimu ya Mapendekezo ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027.
Katika Mwaka wa Fedha 2026/2027, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imepanga kukusanya na kutumia jumla ya shilingi bilioni 72.4 kutokana na vyanzo mbalimbali ikiwemo mapato ya ndani na ruzuku ya Serikali kwa ajili ya kugharamia mishahara (50.6b/=), matumizi ya kawaida yaani 'OC' (5.2b/=), maendeleo (13.8b/=), vyanzo fungiwa kama vile 'CHF', 'User Fee', NHIF, na Michango ya Jamii (2.6b/=).

Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) wakifuatilia kikao kwa umakini.
Akisoma mapendekezo ya rasimu ya bajeti mbele ya DCC, Mkuu wa Divisheni ya Mipango na Uratibu, Francisca Nzota amesema Mwaka wa Fedha 2026/2027, Halmashauri peke yake inakadiria kukusanya na kutumia jumla ya shilingi bilioni 8.4, ambapo shilingi bilioni 5.8 zinatokana na mapato halisi (own source proper) na shilingi bilioni 2.6 kutoka vyanzo fungiwa.
Ili kufanikisha malengo ya Mpango wa Maendeleo katika Mwaka wa Fedha 2026/2027, Halmashauri imekadiria kutumia jumla ya shilingi bilioni 13.8 kwa ajili ya kutekeleza programu na miradi ya maendeleo. Kati ya fedha hizo shilingi bilioni 2.3 ni mapato ya ndani na shilingi bilioni 11.5 ni ruzuku kutoka Serikalini na wadau wengine wa maendeleo.
Mpango wa Maendeleo wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 unalenga kuendeleza juhudi za Serikali katika kuimarisha Halmashauri kwa kujiongezea uwezo wa kutenda kazi, kutathmini na kufuatilia utekelezaji wa mipango ya maendeleo; kuwezesha wananchi kutambua fursa na vikwazo vilivyopo katika maeneo yao ili kupanga na kutekeleza mipango yao; Kuboresha huduma za kijamii na kiuchumi kama ilivyoelezwa katika Dira ya Maendeleo ya Taifa Awamu ya Pili; Kutekeleza miradi ya maendeleo inayoendelea; na kukusanya mapato pamoja kubuni vyanzo vipya.

Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) wakifuatilia kikao kwa umakini.
Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.