Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya (Mbeya DC) leo imefanya kikao cha Kamati ya Watu Wenye Ulemavu Ngazi ya Wilaya, kilichowakutanisha wawakilishi wa makundi mbalimbali ya watu wenye ulemavu.
Lengo la kikao hicho lilikuwa ni kuwapatia na kuwapitisha katika Muongozo wa Uratibu wa Vyama vya Watu Wenye Ulemavu, ili kuimarisha usimamizi na uratibu wa shughuli zao.

Muongozo huo unalenga kuhakikisha vyama na makundi ya watu wenye ulemavu vinatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Sera, Sheria, Kanuni, Miongozo na Taratibu zinazohusu haki, ustawi na maendeleo ya watu wenye ulemavu.
Akiwasilisha taarifa fupi kuhusu muongozo huo wakati wa kikao, Afisa Ustawi wa Jamii kutoka Halmashauri ya Mbeya DC, Bi. Emmiliana Mbisse, alisema kuwa muongozo uliopo sasa unataka mikutano yote ya makundi ya watu wenye ulemavu iratibiwe katika ngazi ya wilaya chini ya usimamizi wa Serikali, kwa kushirikiana na Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) pamoja na wadau wengine.

Alieleza kuwa mikutano hiyo, ikiwemo maadhimisho mahsusi ya vyama kulingana na aina ya ulemavu, inapaswa kufanyika katika ngazi ya Halmashauri. Kwa maadhimisho ya kitaifa, wanachama wa chama kinachoadhimisha watashiriki kupitia Halmashauri zao husika.
Aidha, chama kitahusika kuratibu maadhimisho hayo, huku gharama zikiratibiwa kwa ushirikiano kati ya chama husika, Halmashauri na wadau mbalimbali.
Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.