Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya (Mbeya DC) inatarajia kuanza utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme vijijini kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA) katika vitongoji 114.
Mradi huo unakadiriwa kugharimu shilingi bilioni 3.6, ukilenga kuwawezesha wananchi kupata nishati ya umeme kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kiuchumi na kuchochea maendeleo ya kijamii.
Taarifa hiyo imetolewa na Msimamizi wa Miradi ya REA kutoka Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Mbeya, wakati wa Kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Mbeya DC kilichoketi kujadili na kupitisha Rasimu ya Mapendekezo ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027.
Akizungumza katika kikao hicho, Msimamizi huyo alisema kuwa maandalizi ya awali ya utekelezaji wa miradi hiyo tayari yamekamilika.
“Mikataba ya miradi hii tayari imesainiwa, na mkandarasi wa kusimamia utekelezaji ameshapatikana. Aidha, mkandarasi huyo tayari ameanza kazi katika maeneo yanayopakana na Mbeya DC. Hivyo, tunapaswa kujiandaa mapema kwani kabla ya mwezi huu Februari 2026 kuisha tutaanza rasmi utekelezaji wa miradi katika vitongoji vyote 114 vilivyopo kwenye mpango wa umeme kulingana na bajeti,” alisema.
Kwa upande wake, Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO Wilaya ya Mbeya, Christina Shoki, amewatahadharisha wananchi kuwa makini katika maeneo ambayo miundombinu ya umeme itapita wakati wa utekelezaji wa mradi, ili kuepusha ajali na madhara yanayoweza kujitokeza.
Ameeleza kuwa bado kuna baadhi ya watu wasiokuwa na nia njema wanaojihusisha na hujuma za miundombinu ya umeme, ikiwemo wizi wa mafuta ya transfoma na nyaya za shaba (copper), hali inayohatarisha maisha yao na kuisababishia hasara TANESCO.
“Tabia hii iliwahi kukoma, lakini kwa sasa imeanza kujitokeza tena. Watu wameanza kuiba mafuta ya transfoma pamoja na nyaya za shaba. Vifaa hivi vina umuhimu mkubwa katika uendeshaji wa transfoma. Vinapoibiwa, husababisha mashine kuungua na shirika hulazimika kununua transfoma mpya kwa gharama kubwa. Madiwani mtusaidie kutoa elimu kwa wananchi katika maeneo yenu kuhusu athari za vitendo hivi." alisisitiza Shoki.
Mbaliz Road
Sanduku la posta: 599
Simu ya mezani: 025-2502260
Simu ya mkononi: 0762210758
Baruapepe: ded@mbeyadc.go.tz/info@mbeyadc.go.tz
Copyright ©2018 Mbeya District Coucil . All rights reserved.